Sura mpya za maana kwenye rada za EPL.
LONDON, ENGLAND. MASHABIKI wa Ligi Kuu England wamekuwa na bahati ya kushuhudia mastaa wa maana kwenye ligi hiyo wanaotoka ligi za nje na kwenda kukipiga humo katika miongo michache ya hivi karibuni.
Na hilo linakwenda kutokea tena kwenye dirisha lijalo la majira ya kiangazi ambapo kuna wakali matata kabisa wanaotamba kweye ligi za nje watatua Ligi Kuu England kutokana na klabu kibao kwenye ligi hiyo kuhusishwa na mpango wa kuwasajili.
-Erling Haaland. Hakuna ishu yoyote inayohusu tetesi za usajili zikaacha kuhusiana jina la straika huyo wa Borussia Dortmund. Staa huyo wa Norway amekuwa kwenye rada za timu nyingi ikiwamo Real Madrid na Barcelona - lakini timu za Ligi Kuu England zimekuwa na jeuri ya pesa ambazo zinawapa nafasi kubwa ya kumsajili Haaland, ikiwamo Manchester City, Manchester United, Chelsea na Liverpool ambazo zimekuwa zikihitaji saini ya mchezaji huyo atakayepatikana kwa ada isiyozidi Pauni 68 milioni mwisho wa msimu.
-Rafael Leao. Staa huyo wa AC Milan amekuwa akizivutia klabu nyingi sana za Ligi Kuu England msimu huu. Mbrazili huyo amefunga mabao 10 kutoka wingi ya kushoto huko Italia na Arsenal na Newcastle United wanapambana kuwania saini yake.
-Ronald Araujo. Man United na Liverpool imekuwa ikimfuatilia kwa karibu staa wa Barcelona, Ronald Araujo. Kocha Xavi anahitaji kubaki na beki huyo wa Uruguay hadi mwisho wa mkataba wake mwaka 2023, lakini bado hajakubaliana juu ya dili jipya na hilo linafanya klabu za Ligi Kuu England zimeanza kumfukuzia wakihitaji saini yake.
-Jules Kounde. Chelsea imeonyesha dhamira ya dhati kabisa ya kunasa saini ya beki wa Sevilla, Jules Kounde na bila ya shaka dili lake linaweza kukamilishwa kwenye dirisha la majira ya kiangazi. Baada ya kumkosa kwenye dirisha lililopita, kocha Thomas Tuchel atafanya kila analoweza kunasa saini ya beki huyo kwenye dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
-Ousmane Dembele. Staa wa Barcelona, Ousmane Dembele anajiandaa kuachana na miamba hiyo ya Nou Camp na mara kwa mara amekuwa akihusishwa na klabu za Ligi Kuu England. Chelsea na Arsenal zimekuwa zikihusishwa na huduma yake na huenda mwisho wa msimu akatua EPL.
-Alexander Isak. Arsenal wanahitaji straika mpya na kwa muda mrefu imekuwa ikihusishwa na mkali huyo anayekipiga Real Sociedad. Arsenal ilishindwa kunasa saini yake kwenye dirisha la Januari, hivyo itarudi kumsajili mwishoni mwa msimu huu.