Ujanja wa Southampton washtukiwa.
LONDON, ENGLAND. UNAAMBIWA kushinda mechi kunahitaji mbinu za kijanja. Na hilo linadaiwa kufanywa na Southampton kwenye Ligi Kuu England msimu huu. Na hakika kikosi hicho cha St Mary’s mambo yao yamekuwa yakienda vizuri uwanjani tangu walipokuja na mbinu hiyo mpya.
Mfano mzuri ni kiwango chao cha wiki iliyopita, ambapo walipindua matokeo ya kichapo cha mabao 2-1 na kushinda 3-2 dhidi ya Tottenham.
Ni hivi, wachezaji wa Southampton wameanzisha desturi ya kujiangusha na kuhitaji matibabu ndani ya uwanja kati ya dakika 60 na 70 kwenye mechi zao msimu huu.
Na The Athletic limefanya utafiti na kugundua huo huo ni mpango unaofanywa makusudi na timu hiyo. Utafiti huo umeonyesha kwamba wachezaji wa Southampton waliojiangusha na kuhitaji kutibiwa kati ya dakika 60 na 70 ni 14 katika mechi zao 24 walizocheza kwenye Ligi Kuu England msimu huu. Kila wakati wanapofanya hivyo, wachezaji wamekuwa wakikimbilia nje ya uwanja kupewa vinywaji vya kuongeza nguvu na kupata mapumziko kidogo. Bado haijathibitika kama mastaa wa Southampton wanajiumiza makusudi kusimamisha mchezo.
Vinywaji wanavyopewa vinaripotiwa kuwaongezea nguvu wachezaji, ambao wanaonekana kumaliza mechi dakika za mwisho kwa nguvu sana.
Kuthibitisha hilo, mchezaji Adam Armstrong amedaiwa kuumia mara nne tofauti ndani ya muda huo katika mechi tofauti kukamilisha mpango.
Kwenye mechi ya Spurs, Che Adams aliumia dakika 63, kabla ya Armando Broja naye kuumia na kutaka matibabu yanayochukua dakika kadhaa kwenye dakika 70 baada ya Son Heung-min kufunga bao na kuifanya Spurs kuongoza 2-1. Jambo hilo lilidaiwa kufanya mambo kuwa mazuri, ambapo mabao mawili ya dakika za mwisho kutoka kwa Mohamed Elyounoussi na Che Adams yaliisaidia Saints kupindua matokeo ya kushinda 3-2.
Daktari wa zamani wa Wolves, Phil Hayward aliiambia The Athletic: “Nina hakika wanasayari ya michezo watakuwa wametoa pendekezo la kufanya hivyo na kocha (Ralph) Hasenhuttl amelipitisha.”